Wednesday, November 25, 2009

Papic arejea

Kocha wa Yanga Kostadin Papic amerejea na kuwahi mazoezi ya kwanza ya mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu ya Bara kwenye uwanja wa Uhuru, jijini Dar es salaam.

Mserbia huyo aliondoka nchini kwenda kwao kwa ajili ya mapumziko ya siku saba ya mwisho wa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu na amerejea mara moja kwa ajili ya maandalizi ya Kombe la Tusker na mzunguko wa pili wa ligi.

Papic amerejea akiwa amewautaka uongozi wa klabu hiyo kumchagulia kocha msaidizi mzawa ambaye amewahi kuichezea Yanga na ambaye pia ana cheti cha mafunzo ya awali ya ukocha, jambo ambalo msemaji wa klabu hiyo ya Jangwani Louis Sendeu, amesema kuwa wameyazingatia katika kuchagua majina yaliyopendekezwa kwa ajili ya mchakato wa kumchagua msaidizi huyo.

Kikosi cha Mserbia huyo kimepata nguvu mpya baada ya nyota wake Godfrey Bonny kusema kuwa yuko 'fiti' kuitumikia timu yake katika michuano ya Kombe la Tusker pamoja na michezo ya raundi ya pili ya Ligi Kuu baada ya kuwa nje ya dimba kwa zaidi ya wiki sita kutokana na kusumbuliwa na goti.

Akizungumza na jijini jana, Bonny alisema kuwa kwa kiasi kikubwa maumivu ya goti yaliyokuwa yakimsumbua yamepungua na hata daktari wake amempa nafasi ya kuanza mazoezi mepesi na wenzake.

"Nashukuru Mungu nimepata nafuu kubwa na nimeanza mazoezi mepesi, naamini baada ya wiki moja ama mbili nitakuwa nimerudi kwenye hali yangu ya kawaida na nitaweza kuitumikia timu yangu," alisema Bonny.

SOURCE: nipashe

Friday, November 20, 2009

Wanne waachwa Yanga
Hamisi Yusuf
Mike Barasa
Boniface Ambani

Klabu ya Yanga imewaacha wachezaji 4 katika dirisha dogo la usajili liliofunguliwa kuanzia Novemba mosi mwaka huu.

Wachezaji waliotangazwa kuachwa ni pamoja na mfungaji bora wa mwaka jana Boniface Ambani, beki kutoka Kenya Joseph Shikokoti, Hamis Yusuf na Mike Barasa.

Vincent Barnabas

Mchezaji mwingine Vicent Barnabas ameuzwa kwa mkopo wa miezi 6 kwa timu ya African Lyon.

Monday, November 16, 2009

Yanga vs Prisons leo
Yanga leo inajitupa katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar kupambana na timu ya Prisons ya Mbeya kwenye mchezo wa mwisho wa duru la kwanza la ligi kuu ya Vodacom.

Saturday, November 14, 2009

Kila la heri Baraza
KLABU ya Yanga imeamua kuachana na mshambuliaji wa Kenya, Mike Baraza na imemtakia kila la heri anapokwenda.

Akizungumza na waandishi wa habari makao makuu ya Yanga mtaa wa Twiga na Jangwani jana, Ofisa Habari wa klabu hiyo, Louis Sendeu amekiri kumalizika mkataba na mchezaji huyo, ingawa bado walikuwa wanamhitaji. “Mkataba wetu na Baraza kweli umekwisha na bado tulikuwa tunamhitaji ndio maana tumekuwa tukijaribu kuwasiliana naye ili tufanye mazungumzo, lakini hakuleta ushirikiano hivyo tunamtakia kila la heri huko aendapo.


“Lakini hajafanya vizuri kwa sababu yeye ni mchezaji huru, angekuja tufanye mazungumzo kama angekuwa hataki kurudi tena Yanga si angesema sisi tunamtakia kila la heri licha ya kutoonesha uungwana hakatazwi kwenda kokote,” amesema Sendeu.


Mwanzoni mwa wiki hii mchezaji huyo aliripotiwa kuingia mkataba na Simba ya Dar es Salaam, ambayo ni mpinzani wa jadi na Yanga. Sendeu amesema, nafasi ya Baraza itachukuliwa na John Njoroge aliyekatwa kwenye usajili baada ya Ligi Kuu kuanza. TFF iliitaka Yanga kuondoa jina moja kati ya majina 11 ya wachezaji wa kigeni iliowasajili, ili nafasi hiyo ichukuliwe na George Owino ambaye alihalalishwa kuichezea timu hiyo.


Kuhusu usajili wa dirisha dogo, Sendeu alisema bado kocha Kostadian Papic anaendelea na suala hilo na jana alitarajiwa kumjaribu Sergie Okwundu kutoka Abuja FC ya Nigeria. “Pia anaendelea kumuangalia Salvatory Edward, amemwambia aendelee kuja mazoezini aone kama anaweza kumchukua ama vipi,” alisema.


Alisema pia wamemuuza kwa mkopo Vicent Barnabas kwenda African Lyon atakapocheza kwa miezi sita. “Tutaendelea kumsikiliza kocha nani anamhitaji na nani hamhitaji…tutaendelea kuwauza kwa mkopo ili kupata nafasi ya kusajili wengine,” alisema Sendeu.


Pia alisema baada ya mechi ya keshokutwa dhidi ya Prisons wachezaji watapewa mapumziko ya siku kumi na kwamba kocha Papic atakwenda kwao Serbia kuchukua familia yake.

HABARI LEO

Saturday, November 07, 2009

Mshahara wa Kondic aulizwe Manji

UONGOZI wa klabu ya Yanga umesema hauhusiki na ulipaji wa mshahara wa aliyekuwa kocha wa timu hiyo, Dusan Kondic na anayewajibika na suala ni mfadhili mkuu, Yusuph Manji kama ilivyokuwa katika makubaliano yao.

Kondic ambaye yupo nje ya nchi kwao mara baada ya kuachia ngazi ya kuendelea kukifua kikosi cha Jangwani bado anaidai klabu hiyo mshahara wake wa miezi mitatu ambao hakulipwa.

Afisa habari wa klabu ya Yanga, Louis Sendeu alisema wao kama uongozi hawawajibiki na ulipaji mshahara kwa kocha huyo na hiyo ni jukumu la mfadhili wao ambaye katika mkataba wake ulionyesha yeye mlipa wake atakuwa mfadhili wa klabu hiyo.

Alisema ni kweli kocha huyo anadai kiasi cha shilingi milioni 30 ambazo ni za miezi mitatu, lakini wao hawahusiki katika hilo na hivyo kumwachia mfadhili , Manji kama ilivyokuwa awali.

"Katika jukumu la kumlipa kocha sisi kama uongozi hatuhusiki kwani kocha alipokuja kusaini mkataba ilisaini kuwa analipwa na mfadhili na sisi katika hilo hatuhusiki hivyo hiyo si kazi yetu sisi na endepo atarejea kwa ajili ya kuchukua malipo yake anatakiwa kwenda kwa muhusika na si uongozi,"alisema Sendeu.

Klabu ya Yanga kwa sasa inanolewa kocha Kostadin Papic ambaye amechukua nafasi ya Kondic aliyeiacha klabu hiyo

MWANANCHI

Saturday, October 31, 2009

Tumelala 1-0

Bao pekee la mchezo liliofungwa na Musa Hassan Mgosi leo limetutoa katika Uwanja wa Taifa vichwa chini baada ya Simba kuendeleza wimbi lake la ushindi na sasa kufikisha pointi 30 katika michezo 10.
Mgosi alifunga bao hilo baada ya kupewa pasi na Danny Mrwanda katika dakika ya 26. Hata hivyo Mrwanda hakumaliza mchezo huo baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu katika dakika ya 68.
Hongera kwa walioshinda, ligi inaendelea.
Yanga vs Simba

Macho na masikio ya maelfu ya mashabiki wa soka nchini leo yataelekezwa kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya soka ya Tanzania Bara kati ya vigogo vya soka hapa nchini Simba na Yanga.

Huo utakuwa ni mchezo wa pili kwa vigogo hivyo kukutana ndani ya mwaka huu, ambapo mara ya kwanza ilikuwa ni Aprili 19 katika mchezo uliochezwa kwenye uwanja huo na timu hizo kwenda sare ya 2-2, ambapo Yanga ilikuwa na jukumu la kusawazisha.

Mchezo wa leo utakuwa na umuhimu mkubwa kwa Yanga kutokana na ukweli ina changamoto kadhaa za kukabiliana nazo.

Kocha mpya, Kostadin Papic aliyechukua mikoba kutoka kwa Dusan Kondic atakuwa anakalia benchi la timu hiyo kwa mara ya kwanza wiki tatu zilizopita.

Pia Yanga yenye pointi 18 itakuwa na kibarua cha kupunguza kasi ya Simba, ambayo inaongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 27 baada ya kushinda mechi zake tisa za mwanzo.

Kutokana na ukweli kuwa ikipoteza mchezo huo ina maana itazidi kutoa mwanya kwa Simba kuzidi kupaa katika msimamo wa ligi hiyo. Yanga itakuwa fursa kwao kuendeleza ubabe wa kuifunga Simba kwa mara ya pili kwenye uwanja huo kama ilivyofanya katika raundi ya kwanza ya Ligi Kuu msimu uliopita, ambako Yanga ilishinda bao 1-0, Oktoba 26,2008.

Katika mchezo huo, Simba itakuwa na kazi moja tu ya kuhakikisha wanaendeleza wimbi la ushindi kwenye michezo yake ya ligi pamoja na kutaka kuweka rekodi mpya ya kushinda michezo 10 mfululizo.

Akizungumzia mchezo huo, kocha wa Yanga, Kostadin Papic alisema kuwa mara baada ya kukirekebisha kikosi chake ana matumaini ya kufanya vizuri kwenye mchezo huo.

Kwa upande wake, kocha wa Simba, Patrick Phiri aliweka wazi kuwa anachohitaji ni pointi tatu kutoka kwa Yanga na uhakika wa kuzipata pointi hizo anao.

Tuesday, October 27, 2009

Tibaigana awafungulia akina Maftah

WACHEZAJI Amir Maftah na Moses Odhiambo wa Yanga, wako huru kuichezea timu yao kwenye mpambano wa Jumamosi dhidi ya Simba baada ya kufutiwa kifungo cha kukosa mechi tatu na faini ya shilingi 500,000 baada ya kikao cha kamati ya nidhamu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Kushindwa kuwasilishwa kwa aina ya matusi waliyotukanwa na wachezaji hao ni moja ya sababu za kuachiwa huru na kufutiwa faini ambayo ilitakiwa kulipwa na wachezaji hao.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa kamati hiyo Kamishna wa Polisi Mstaafu, Alfred Tibaigana alisema kamati yake imeshindwa kugundua kosa na kutoa maamuzi ya kuwapa uhuru wachezaji hao kwa kushindwa kugundua sababu halisi ya makosa waliyoshitakiwa.

''Hukumu inaonyesha kuwa wachezaji hao walimtukana msaidizi wa mwamuzi wa kwanza mara baada ya mpira kumalizika na taarifa hizo zikaandikwa kwa taarifa ya kamisaa,''alisema Tibaigana.

''Hukumu ambayo bado haina uhakika kwa kuwa walishindwa kuandika aina ya matusi ambayo yalitukanwa na wachezaji hao, na sisi kama kamati hukumu za namna hiyo huwa tunazihukumu kwa kumpa haki mshatakiwa kwa kuwa zinakuwa za shaka kwa kutokamilika.

''Itakuwa bora yanapotokea matatizo kama hayo , basi waamuzi wanapoandika ripoti zao wanatakiwa kuandika aina ya matusi ambayo wanatukanwa kwa kuwa wao ni binadamu na tukio kama hilo halikuwa na ushahidi,'' alieleza Kamanda Tibaigana.

Alisema wao kama kamati ya mashindano wamewaachia huru wachezaji hao tangu kufanyika kwa kikao hicho kilipokutana na kubaini kushindwa kwa waamuzi na kamisaa kuweka bayana matusi kutambua makosa kazi ambayo wamewaachia TFF kama itakatwa rufaa nyingine.

Kutokana na uamuzi huo, Maftah na Odhiambo waliotiwa hatiani na kupewa adhabu na faini hiyo wakidaiwa kumtukana mwamuzi siku ya mchezo baina ya Yanga na Azam FC mchezo uliomaliza kwa suluhu ya bao 1-1, wameondolewa kifungoni.