Kocha wa Yanga Kostadin Papic amerejea na kuwahi mazoezi ya kwanza ya mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu ya Bara kwenye uwanja wa Uhuru, jijini Dar es salaam.
Mserbia huyo aliondoka nchini kwenda kwao kwa ajili ya mapumziko ya siku saba ya mwisho wa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu na amerejea mara moja kwa ajili ya maandalizi ya Kombe la Tusker na mzunguko wa pili wa ligi.
Papic amerejea akiwa amewautaka uongozi wa klabu hiyo kumchagulia kocha msaidizi mzawa ambaye amewahi kuichezea Yanga na ambaye pia ana cheti cha mafunzo ya awali ya ukocha, jambo ambalo msemaji wa klabu hiyo ya Jangwani Louis Sendeu, amesema kuwa wameyazingatia katika kuchagua majina yaliyopendekezwa kwa ajili ya mchakato wa kumchagua msaidizi huyo.
Kikosi cha Mserbia huyo kimepata nguvu mpya baada ya nyota wake Godfrey Bonny kusema kuwa yuko 'fiti' kuitumikia timu yake katika michuano ya Kombe la Tusker pamoja na michezo ya raundi ya pili ya Ligi Kuu baada ya kuwa nje ya dimba kwa zaidi ya wiki sita kutokana na kusumbuliwa na goti.
Akizungumza na jijini jana, Bonny alisema kuwa kwa kiasi kikubwa maumivu ya goti yaliyokuwa yakimsumbua yamepungua na hata daktari wake amempa nafasi ya kuanza mazoezi mepesi na wenzake.
"Nashukuru Mungu nimepata nafuu kubwa na nimeanza mazoezi mepesi, naamini baada ya wiki moja ama mbili nitakuwa nimerudi kwenye hali yangu ya kawaida na nitaweza kuitumikia timu yangu," alisema Bonny.
SOURCE: nipashe





